MATUKIO ya ukatili dhidi ya watoto, bado yameendelea kushika kasi
kwenye maeneo mbalimbali nchini ambapo katika Mkoa wa Simiyu, mtoto
mwenye umri wa miaka 17 (jina tunalihifadhi), mkazi wa Bariadi Mjini na
mwanafunzi wa Shule ya Msingi Bariadi, amejikuta akifungwa minyororo
mikononi na miguuni kwa miezi minne nyumbani kwa mganga wa kienyeji.
Mganga huyo amefahamika kwa jina la Mdeli Msanja ambaye aliamua
kufanya ukatili huo baada ya wazazi wa mtoto huyo ambaye anamatatizo ya
akili, kushindwa kumlipa pesa za matibabu.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoani humo, Charles
Mkumbo, alisema wazazi wa mtoto huyo walikubaliana na mganga huyo
kumlipa sh. 260,000 kama mtoto wao atapatiwa matibabu na kupona.
“Pamoja na wazazi kukubaliana
na mganga husika, hali ya mtoto haikuweza kubadilika wala kupata unafuu
hivyo waliomba kumchukua mtoto wao kitendo ambacho kilipingwa na mganga
kwa madai ya kutolipwa pesa zake ambazo walikubaliana,” alisema.
Alisema mganga huyo aliamua kumchukua mtoto huyo na kumfungia
chumbani kwake kwa minyororo miguuni na mikononi kwa kipindi cha miezi
minne akidai pesa zake na kuwapa wakati mgumu wazazi wake.
Kutokana na msimamo wa mganga huyo, mama mzazi wa mtoto huyo Malita James (46), alilazimika kwenda kutoa taarifa Kituo cha Polisi Bariadi kuhusu mateso anayoyapata mwanaye kwa mganga.
“Polisi walishirikiana na
Dawati la Jinsia kufanya uchunguzi wa tukio hili na walipofika kwa
mganga, walimkuta akiwa amemfunga minyororo miguuni na mikononi,” alisema Kamanda Mkumbo.
Aliongeza kuwa, polisi walimkamata mganga huyo ambaye hakuwa na kibali cha kutoa tiba za asili, pia alikamatwa na nyara za Serikali ambazo ni pembe moja ya swala na mikia miwili ya nyumbu ambapo uchunguzi ukikamilika atafikishwa mahakamani.
No comments:
Post a Comment