Simplfy language

thanx

Friday, May 23, 2014

Wananchi wamlipua Lissu kwa Kinana...


Wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki, wamemuomba Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, awasaidie kutatua kero zinazowakabili za barabara, elimu na afya.
Wananchi hao wamedai hatua ya kumuomba Kinana awasaidie inatokana na Mbunge wao, Tundu Lissu (Chadema), kuwakataza kuchangia miradi ya maendeleo hali iliyosababisha miradi ya ujenzi wa shule na zahanati kusimama kwa kipindi cha miaka minne.Wakizungumza jana wilayani Ikungi mkoani Singida, mbele ya Kinana, wananchi hao walisema Mbunge huyo amekuwa akiwakataza kuchanga fedha kwa ajili ya kujenga madarasa na majengo ya zahanati kwa madai kuwa serikali ina fedha za kutosha za kufanya kazi hizo.“Ndugu Kinana tunaomba utusaidie kwani tangu tulipomchagua Mbunge wetu, Tundu Lissu, hajaendeleza miradi ambayo ilianza kufanywa na Mbunge wa CCM aliyepita, baada ya yeye kutukataza kuchanga aina yeyote ya michango itakayotakiwa na halmashauri kwa ajili ya maendeleo, tumeendelea kuwa katika hali ya ufukara” alisema Omary Lissu mkazi wa kijiji cha Unyanghumpi.Alisema tangu wamekatazwa kutoa fedha za miradi hakuna kazi ambayo imeendelea hasa katika zahanati Kimbwi ambayo walitarajia iwe imeanza kutumika tangu mwaka 2011 lakini hadi sasa bado haijakamilika na kwamba diwani wao amekuwa akiwashinikiza kutoshiriki shughuli hizo.Naye Mwalimu wa Shule ya Msingi Unyanghumpi, Juliana Joseph, ambaye anafundisha darasa la awali, alisema tangu madarasa hayo yajengwe kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, mpaka sasa hakuna majengo mengine mapya wala ya zamani kumaliziwa hali inayowafanya baadhi ya wanafunzi kusoma katika darasa ambalo halijaezekwa.“Ni mwaka wa nne nafundisha katika darasa hili ambalo halina paa,  na mvua inaponyesha inatubidi tusiudhurie vipindi. Mbunge wetu na diwani walitoa tamko la kuwataka wananchi wasichangie umaliziaji wa jengo ndiyo maana hadi sasa tuko hapa, wala hajawahi kufika kutoa msaada wowote,” alisema Joseph.Alisema darasa la awali lina jumla ya wanafunzi 135 ambao wote wanakaa kwenye vumbi kwani hakuna madawati na vifaa vingine kama dhana za kufundishia.Mkazi mwingine alisema wamekuwa wakipata tabu ya kufuata huduma ya afya katika kijiji kingine wakati kijijini hapo kuna zahanati ambayo imejengwa inasubiri kukamilika.Akizungumza na wananchi hao katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Makyungi, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema kiongozi bora ni yule anayechangia maendeleo ya wananchi na siyo kuwakataza wananchi kufanya maendeleo.Alisema Tundu lissu anafanya mambo ambayo hayaendani na matarajio ya wananchi kwani walimchagua wakiamini ataleta maendeleo badala yake anazuia maendeleo.Kwa upande wake, Kinana, alimtaka Lissu kuacha porojo za majukwaani na arudi kwa wananchi kuwatimizia ahadi alizotoa kwani anafedha nyingi anazopatiwa bungeni.Alisema wilaya ya Ikungi iko nyuma kimaendeleo ikilinganishwa na wilaya nyingine nchini sababu kubwa ikiwa ni mbunge mwenyewe ambaye ameshindwa kupigania maendeleo ya jimbo lake na badala yake amekuwa akigombana na kila mtu serikalini.MAJIBU YA LISSUNIPASHE lilipomtafuta, Tundu Lissu, ili kujua sababu ya kuwakataza wananchi wake kutoa michango ya miradi ya maendeleo jimboni kwake, alisema amefanya hivyo kwani hakuna sheria zinazomtaka mwananchi achangie miradi ambayo ni kazi ya serikali.Alisema shule na zahanati zinazojengwa ni za serikali na kwamba Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alishatangaza bungeni kuwa, serikali imetenga fedha kwa ajili ya kujenga maabara katika shule zote za serikali, hivyo hawezi kuruhusu fedha za wananchi wake ziliwe na wajanja."Wanaokataa kuchanga fedha ni wale ambao wananiunga mkono mimi kwani wakati nawaomba kura niliahidi kuwafutia michango yote wanayochangishwa na serikali ambayo inaliwa na watendaji wa serikali za mitaa, hatuwezi kuchanga hela wakati serikali ina uwezo wa kujenga maabara na zahanati kama ilivyo ahidi," alisema Lissu.
 

No comments:

Post a Comment